http://tanzanianewz.blogspot.com
Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Robert Manumba amestaafu rasmi utumishi wa umma baada ya kufikia umri wa kustaafu kisheria wa miaka 60.
Dar es Salaam. Mkurugenzi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai (DCI), Robert Manumba amestaafu rasmi utumishi wa umma baada ya kufikia umri wa kustaafu kisheria wa miaka 60.
Manumba aliyeanza kulitumikia Jeshi la Polisi
miaka ya 1970, nafasi yake itashikwa kwa muda na Mkuu wa Ufuatiliaji na
Tathmini (CID), Kamishna Isaya Mungulu.
“Wakati utaratibu wa uteuzi wa Mkurugenzi wa
Upelelezi ukiendelea, Kamishna Mungulu, atakaimu nafasi hiyo,” ilisema
sehemu ya taarifa ya Polisi kwa vyombo vya habari iliyotolewa jana na
Msemaji wake, Advera Senso.
Akizungumzia kustaafu huko, Inspekta Jenerali wa
Polisi (IGP) Said Mwema, amemshukuru na kumpongeza Manumba kwa weledi na
uaminifu mkubwa aliouonyesha wakati wote alipokuwa mtumishi wa Jeshi la
Polisi.
Amemtaka aendelee kuwa msaada kwa jeshi hilo kwa
kutoa ushirikiano wa namna yoyote ile unaoweza kusaidia kupunguza
uhalifu nchini akisema usalama ni taaluma kama zilivyo nyingine.
Historia yake kikazi
Katika utumishi wake, DCI Manumba amelitumikia
jeshi hilo katika nyadhifa mbalimbali zikiwamo katika Chumba cha Kupokea
Mashtaka kati ya mwaka 1976 hadi 1977 na baadaye Mwendesha Mashtaka
Wilaya ya Kibondo na Kasulu mkoani Kigoma kati ya 1977 na 1984.
Alikuwa Mkufunzi katika Chuo cha Polisi kilichopo
Kurasini Dar es Salaam, kati ya mwaka 1984 na 1987 kabla ya kuteuliwa
kuwa Mkuu wa Upelelezi Wilaya ya Kipolisi ya Magomeni na Kinondoni.
Manumba baadaye aliteuliwa kuwa Naibu Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Dar
es Salaam kuanzia 1987 hadi 1993.
Kati ya mwaka 1993 na 1995, alikuwa Mkuu wa
Upelelezi wa Mkoa wa Arusha kabla ya kuteuliwa kushika wadhifa wa
Mkufunzi Mkuu wa Chuo cha Polisi Moshi kati ya 1995 na 1996.
Aliteuliwa kuwa Mkuu wa Kitengo cha Kukabiliana na
Uhalifu wa Kughushi Makao Makuu ya Upelelezi mwaka 1996 na 1997 na
baadaye kuwa Mkuu wa Kitengo cha Usalama, Intelijensia na Kupambana na
Biashara ya Dawa za Kulevya kwenye Makao Makuu ya Upelelezi kuanzia 1997
hadi 2001.
Mwaka 2001 hadi 2006 aliteuliwa kuwa Mkurugenzi
Msaidizi wa Upelelezi wa Makosa ya Jinai na kuanzia mwaka 2006 hadi
anastaafu, alikuwa Mkurugenzi wa idara hiyo.
Mapema Januari, jina la DCI Manumba lilitawala
vyombo vya habari baada ya hali yake kuwa mbaya na kulazwa katika Chumba
cha Wagonjwa Mahututi (ICU), Hospitali ya Aga Khan, Dar es Salaam
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni